Hakiki riwaya ya Fedheha kwa kigezo cha nadharia, fani na maudhui.



SWALI:          Hakiki riwaya ya Fedheha kwa kigezo cha nadharia, fani na maudhui.
UHAKIKI WA RIWAYA YA FEDHEHA
Jina la kitabu Fedheha linasadifu yaliyomo kwani kwa tafsiri ya kawaida neno fedheha linamaanisha aibu aipatayo mtu. Kwa hali hiyo basi jina la kitabu linaendana na yaliyomo kama ifuatavyo:-
·         Khalfani alifedheheshwa baada ya kujulikana/ kusemekana sababu iliyopelekea kwenda mahabusu ni kukutwa na shoga nyumba ya kulala wageni. (Uk. 62)
·         Fedheha nyingine ilijitokeza pale Baisar uovu wake ulipobainishwa na kuwekwa wazi kuwa alijihusisha na uuzaji na usafirishaji wa madawa ya kulevya na kumiliki danguro. (Uk. 87, 105-106)
·         Pia Khalfani alifedheheshwa na mkewe Latipha kuolewa na Baisar. Vilevile Baisar kumtumia Latipha kusafirisha madawa ya kulevya. (Uk.36)
·         Fedheha nyingine inaonekana kupitia mama yake Khalfani baada ya kusukumwa na askari mbele ya mwanae na kuanguka chini. (Uk. 29)











Utangulizi
Riwaya hii ya Fedheha imeandikwa na George Iron Mosenya, kwa ujumla inahusu mkasa wa kimapenzi kati ya Khalfani Masoud na Latipha ambapo mkasa huu wa kimapenzi unaibua masuala mengine mazito kama uuzaji wa madawa ya kulevya, usaliti katika ndoa na umiliki wa biashara ya danguro.
Ufuatao ni uhakiki wa riwaya ya fedheha kwa kutumia kigezo cha fani na maudhui.
Maudhui
1.      Dhamira kuu.
Mapenzi na ndoa, dhamira hii kwa sehemu kubwa imepelekea kuibuka kwa masuala mengine yaliyojadiliwa na mwandishi katika riwaya hii. Pia mwandishi ameonesha kuwepo kwa mapenzi ya kweli na yasiyo ya kweli.
Mapenzi ya kweli yanajitokeza kati ya Khalfani Masoud na Geza Ulole ambapo Geza alikubali kutumia muda wake mwingi kutatua tatizo lililokuwa linamkabili Khalfani katika kujua ukweli juu ya mke wake Latipha
Mapenzi mengine ya dhati yanajitokeza pale Geza Ulole anapoonesha moyo wa uzalendo baada ya kuwaokoa abilia wenzake wakati walipotekwa na majambazi. (Uk. 38)
Khalfani alionesha mapenzi ya dhati kwa Latipha.
Mapenzi yasiyo ya kweli mwandishi anayabainisha kupitia Latipha kwa Khalfani. (Uk. 16)
Latipha kuolewa na bwana mwingine. (Uk. 34)
Pia Lolita kumsaliti Geza Ulole.




Dhamira ndogondogo.
i.                    Usaliti,
Mwandishi ameonesha jambo hili kupitia mhusika Latipha kumsaliti Khalfani kwa kuolewa na Baisar (Uk. 16). Vilevile usaliti mwingine unajitokeza kupitia mhusika Lolita kumsaliti mpenzi wake Geza Ulole kwa kuolewa na mwanaume mwingine.
ii.                  Rushwa,
Suala hili limejitokeza baada ya Geza kutoka gerezani na kukuta mama yake amekufa na chanzo cha kifo chake ni kuwa mwarabu (Baisar) amehusika (Uk. 60 na 87)
iii.                Uongozi mbaya,
Suala hili limejitokeza kupitia vigogo wakubwa wa Serikali pamoja na vyombo vya dola ambapo walishirikiana na wahalifu kuwatesa wanyonge (Uk. 60) mwandishi amesema kuwa Baisar alikuwa na pesa, pesa hizo alizifanya fimbo kwa wanyonge. (Uk. 87)
iv.                Biashara haramu,
Suala la madawa ya kulevya, jambo hili limebainishwa na mwandishi anapomtumia mhusika Baisar kuwa alikuwa akijihusisha na biashara hiyo kwa kutumia mabinti. (Uk. 87, 105)
Suala la uuzaji wa miili (Danguro), mwandishi ameonesha kuwepo kwa biashara ya uuzaji wa miili ya wasichana maskini ambapo ilimilikiwa na Baisar. (Uk. 87)
v.                  Uvumilivu,
Mwandishi ameonesha dhamira hii kupitia mhusika Khalfani kwani ameonesha uvumilivu wa hali ya juu kulinda penzi lake kwa Latipha (Uk. 36)
vi.                Matabaka,
Mwandishi amebainisha kuwepo kwa suala hili la walionacho na wasionacho kama mke wa Baisar alipotekwa vyombo vya habari vilitangaza lakini watu wengine walipotekwa kama Latipha hakuna aliye andika habari hii kwa kuwa wao ni maskini. (Uk. 76)
vii.              Wivu,
Mwandishi kaonesha kuwepo kwa dhamira hii akimhusisha mhusika mkuu Khalfani kuonesha hali ya wivu juu ya mkewe Latipha, wakati aliposikia mlio wa simu ya mke wake kwenye daladala. (Uk. 2)

viii.            Umoja na mshikamano,
Dhamira hii imebainishwa kwa kuwatumia wahusika Khalfani na Geza Ulole waliposhirikiana tangu walipo fahamiana na haatimaye kupelekea kupatikana kwa Latipha na kufungwa kwa Baisar na mke wake. (Uk. 31)
ix.                Ujasiri na kujitoa mhanga,
Mwandishi amebanisha kuwepo kwa dhamira hii kwa kumtumia Geza Ulole alipojitoa mhanga kwa kuwaokoa abiria wenzake wakiwa safarini toka Mwanza kuelekea Dar  es  Salaam. (Uk. 38)
x.                  Ukosefu wa haki,
Mwandishi amejadili dhamira hii kupitia mhusika Khalfani akionesha kutuhumiwa kwa kesi asizozifahamu pia hakupewa muda wa kujitetea. (Uk. 29)
xi.                Nafasi ya mwanamke katika jamii,
Mwandishi amemchora mwanamke katika nafasi mbalimbali kama:-
Msaliti wa ndoa, mwandishi amemtumia Latipha katika suala hili.
Kama mlezi, mwandishi amemuonesha mhusika mama Latipha kama mama mwenye malezi mabaya katika kumlea mwanae Latipha.
Vilevile mwandishi amemuonesha mama Khalfani kama mama mwenye malezi mabaya na asiye penda kusikiliza maelezo yoyote kutoka kwa mwanae Khalfani.
Mwanamke amechorwa kama chombo cha starehe, kwa kumuonesha mama Latipha kumstarehesha Baisar.
Mwandishi amemwelezea mwanamke kama mwenye kushiriki uovu, msanii ameonesha haya kwa kumtumia mhusika Mozah kuonekana akishirikiana na mume wake (Baisar) kumtunzia siri.
Kama jasiri, mtunzi ameonesha haya kwa kumtumia mke wake Baisar alipopambana na Khalfani kama njia ya kujiokoa nyumbani kwa Geza.
Kama msomi, kwa kuwatumia Latipha na Mariamu kuwa ni wanafunzi wa Chuo Kikuu.
Asiye na msimamo, mwandishi amebainisha hili kupitia mhusika Latipha hakuwa na msimamo wa kuitetea ndoa yake na kuamua kuolewa na Baisar.
Kama mwongo, mwandishi amemwonesha Latipha akimdanganya mume wake Khalfani kuwa anataka kugombea mashindano ya umiss Chuo.
2.      Ujumbe.
i.                    Umoja na ushirikiano ni nguzo bora katika utatuzi wa matatizo mbalimbali.
ii.                  Ni vizuri kupembua ushauri tunaopewa na ndugu na jamaa zetu.
iii.                Usaliti kwa wanandoa na wapenzi haufai na mwisho wake ni mbaya.
iv.                Ni vizuri kujiepusha na biashra haramu (Uuzaji wa madawa ya kulevya na umiliki wa danguro)
v.                  Ni vizuri kumsikiliza mtoto katika matatizo yanayomkabili.
vi.                Unapotafuta haki yako usikate tamaa.
vii.              Ofisi na taasisi za umma zitende haki bila kujali tofauti zetu.
viii.            Usilazimishe mapenzi kwa mtu asiye kupenda.
ix.                Wivu kupita kiasi katika mapenzi haufai
x.                  Si vizuri kwa wazazi kuchangia kuvunja ndoa za watoto wao.
xi.                Mwanaume ni kiungo muhimu katika familia.

3.      Falsafa.
Mwandishi anaamini kuwa, ili jamii yoyote iweze kuwa na mabadiliko chanya na yenye usawa kwa wote, ni lazima iondokane na mambo yote yanayokwamisha ujenzi wa jamii mpya endelevu kama:- Rushwa, uuzaji wa madawa ya kulevya, usaliti, malezi mabaya na ubaguzi.

4.      Msimamo.
Msanii anamsimamo wa kiyakinifu kwani ameyabainisha matatizo yanayoikabili jamiii kama:-  usaliti, uuzaji wa madawa ya kulevya, uuzaji wa miili (danguro) na pia ameonesha njia za utatuzi wake kama kushitakiwa na kufungwa kwa Baisar na mke wake.

5.      Mtazamo.
Mwandishi anamtazamo wa kimapinduzi kwani ameonesha na kubanisha mapambano na mgongano wa kitabaka uliopo kati ya tabaka la juu na tabaka la chini, mambo ambayo ni halisi katika jamii zetu.
6.      Itikadi.
Mwandishi ameegemea kwenye jamii yake kwani ameonesha mambo mbalimbali yanayolikabili tabaka tawaliwa kama vile suala la rushwa,uongozi mbaya, unyanyasaji na uuzaji wa madawa ya kulevya.

Fani.
1.      Muundo.
Muundo hujimwisha sura, msuko, mandhari na wahusika.
i.                    Sura,
Mwandishi wa riwaya hii amegawanya kazi yake katika sura kumi na tisa (19). Sura ya 1-3 zinazungumzia mapenzi na ndoa ya Khalfani Masoud na Latipha, wivu na migogoro ya ndoa kati yao. Sura ya 4 - 6 zinazungumzia kupotea kwa Latipha, kukamatwa kwa Khalfani, kupelekwa mahabusu na kutolewa kwake. Sura ya 7 – 9 Geza na Khalfani kusimuliana mapito yao, kwenda ukumbini kubainisha/ kutafuta chanzo cha tatizo. Sura ya 10 -13 kubainisha adui yao na kupanga mbinu za kupambana  naye. Sura ya 14 – 16  kupanga mipango ya kuingia kwa Baisar, kumteka mke na watoto wake. Sura ya 17 – 19 kurudi tena kwa Baisar kutoa vitisho, kupambana na Baisar na hatimaye Baisar na mkewe kufungwa.
ii.                  Msuko,
Mwandishi ameonesha mpangilio wa visa na matukio ni wa moja kwa moja kwani anabainisha tangu matukio yanaanza mpaka yanakamilika. Mwandishi ameonesha Khalfani anaanza mahusiano na Latipha, ndoa yao, Khalfani kwenda mahabusu, kukutana na Geza Ulole, kutafuta mbinu za kupambana na Baisar, kumpata Latipha na kufungwa kwa Baisar na mke wake.

iii.                Mandhari,
Mazingira halisi ya Kitanzania, mandhari ya Dar es Salaam, Mwanza na Morogoro.
·         Dar es Salaam muktadha wa Koko beach (Uk. 7) Mbezi Africana (Uk. 82), Temboni, Chuoni (Chuo cha Uhasibu), Hospitali ya Magomeni  (Uk. 25), kwenye daladala (Uk. 3).
·         Mwanza muktadha wa mahabusu (Uk. 31 na 38).
·         Morogoro muktadha wa nyumba ya kulala wageni (Uk. 100).

iv.                Wahusika,
Khalfani.
Ø  Mhusika mkuu.
Ø  Mume wa Latipha.
Ø  Mwenye wivu kwa mkewe.
Ø  Jasiri.
Ø  Mvumilivu.
Ø  Ana mapenzi ya dhati kwa mkewe.
Ø  Msomi wa Chuo Kikuu.
Ø  Mtoto wa mama Khalfani.
Ø  Anafaa kuigwa na jamii.
Geza Ulole ( Iga ufe).
Ø  Rafiki wa Khalfani.
Ø  Mtu wa kisasi.
Ø  Jasiri.
Ø  Mvumilivu.
Ø  Mshauri mzuri.
Ø  Mbabe  (Uk. 31)
Ø  Alikuwa mpenzi wa Lolita.
Ø  Anafaa kuigwa kwa baadhi ya mambo.
Latipha.
Ø  Mke wa Khalfani na Baisar.
Ø  Hana mapenzi ya kweli kwa Khalfani.
Ø  Msomi wa Chuo Kikuu.
Ø  Msaliti wa ndoa.
Ø  Mwongo.
Ø  Msafirishaji wa madawa ya kulevya.
Ø  Hafai kuigwa na jamii.
Baisar.
Ø  Ni mume wa Mozah Baraghashi.
Ø  Baba wa watoto wawili.
Ø  Mwarabu.
Ø  Mfanyabiashara wa madawa ya kulevya na mmiliki wa danguro.
Ø  Anashirikiana na vigogo Serikalini kuumiza wanyonge.
Ø  Malaya.
Ø  Hafai kuigwa na jamii.
Mama Latipha.
Ø  Mama mzazi wa Latipha.
Ø  Alishiriki kuvunja ndoa ya bintiye.
Ø  Ni hawala wa Baisar.
Ø  Mama mkurupukaji.
Ø  Ana vitisho.
Ø  Hafai kuigwa na jamii.
Mama Khalfani.
Ø  Mzazi wa Khalfani.
Ø  Hapendi kumsikiliza mwanae.
Ø  Hachambui kila anachokisikia.
Ø  Hafai kuigwa na jamii.
Wahusika wengine ni kama:- Mariam, Lolita, Jemsi, John na Michael.

2.      Mtindo.
Mbinu za kiuandishi.
·         Mwandishi ametumia herufi kubwa kwa kila neno la kwanza mwanzoni mwa kila sura.
·         Ametumia mbinu ya masimulizi na kwa sehemu chache ametumia mbinu ya majibizano. Mfano, Majibizano kati ya Khalfani na Baisar (Uk. 98), majibizaqno kati ya Geza na Khalfani (Uk. 51).
·         Pia mwandishi ametumia mbinu ya ndoto katika kazi yake, ambapo ndoto hiyo iliotwa na Khalfani (Uk. 20- 21).
Matumizi ya lugha.
Kwa ujumla lugha iliyotumiwa na mwandishi ni nyepesi, fasaha na yenye kueleweka kwa wasomaji wake. Yafuatayo ni matumizi ya lugha kama yalivyojitokeza katika riwaya hii:-



i.                    Misemo.
Baadhi ya misemo iliyojitokeza ni kama:-
a)      Mapenzi yananipeleka puta (Uk. 2)
b)       Funika kombe mwanaharamu apite (Uk. 7)
c)      Mtu mzima dawa (Uk. 8)
d)     Kulivalia njuga (Uk. 8)
e)      Mtoto hakui kwa mamae (Uk. 28)
f)       Kutwanga maji kwenye kinu (Uk. 20)
g)      Usihukumu ladha ya kitabu kwa kutazama jalada lake (Uk. 65)
h)      Vizuri huliwa na wengi (Uk. 41)
i)        Umbali hunyausha mapenzi (Uk. 9)

ii.                  Methali.
a)      Hayawi hayawi hatimaye yakawa (Uk. 8)
b)      Mkuki kwa nguruwe kwa binadamu mchungu (Uk. 84)

iii.                Nahau.
a)      Nikaukata mzizi wa fitina (Uk. 23)
b)      Niko chini ya miguu yako (Uk.28)
c)      Yule boya hana kifua (Uk. 81)
d)     Kukata shauri (Uk. 39)
e)      Bega kwa bega (Uk. 84)
Tamathali za semi
i.                    Tashibiha,
a)      Aliendelea kuwa mbele na mimi nyuma kama mkia (Uk. 49)
b)      Moyo ukipiga hodi kwa nguvu kifuani kama unaosisitiza kuwa unataka kutoka nje kupunga upepo (Uk. 37)


ii.                  Tashihisi,
a)      Harufu iliyonipokea pale iliupasua moyo wangu kwa hofu (Uk. 3)
b)      Nilifumba macho nikauma meno yangu kisha nikaitazama mikono yangu jinsi ilivyo shindana kutokwa jasho (Uk. 14)
c)      Ile hasira ikaondoka na uwoga wangu (Uk. 71)
d)     Kauli hizi zilizopita katika kichwa changu ziliniumiza sana kiasi kwamba niliusikia moyo ukipiga hodi kwa nguvu kifuani kama unasisitiza kuwa unataka kutoka nje kupunga upepo (Uk. 37)
e)      Mkojo ukabisha hodi (Uk. 74)

iii.                Tashititi,
a)      Latipha mke wangu una wazimu, nikamuuliza huku nikimtazama usoni (Uk. 12)
b)      Huyu ndiye mume wake ama? (Uk. 42)
c)      Waliniona nimekabwa kisha nikapigwa vibaya sana, halafu wananiuliza kitu gani kimetokea (Uk. 26)

iv.                Tafsida,
a)      Michael huku akiondoka kuelekea msalani (Uk. 5)
b)      Mambo yaliyokuwa yanafanywa nao wakiwa faragha (Uk. 7)

v.                  Misimu,
a)      Kesho kitanuka mjini hapatakalika (Uk. 76)
b)      Zoba (Uk. 60)
c)      Boya (Uk. 81)

vi.                Kejeli,
a)      Marashi gani hayo nimeyapenda sana nilimsanifu (Uk. 11)
b)      Kina Latipha wapo wengi au kesho nikuletee Latipha mpya uoe fasta fasta Geza alinihoji kimasihara huku nikicheka (Uk. 45)

Mbinu za kisanaa.
i.                    Takriri,
a)      Kilevi levi (Uk. 5)
b)      Kimya kimya (Uk. 3)
c)      Ama hakika dhaifu ni dhaifu tu (Uk. 90)
d)     Fasta fasta (Uk. 45)
e)      Geza alikoroma, alikoroma,alikoroma  (Uk. 90)
f)       Nikawa nikibofya bofya simun yangu (Uk. 38)
g)      Mimi namuua, namuua nasema (Uk. 88)

ii.                  Mdokezo,
a)      Wanaume wengine ……… yaani mimi kaka nikija  …… ( Uk. 7)
b)      Halafu umesema uponaye katika dili gani we si ulise …….. (Uk. 50)
c)      Baisar na  …… na ……. (Uk. 77)
d)     Huyu bwana anaratibu mashindano ya urembo kisha …… kisha ….. (Uk. 22)

iii.                Nidaa,
a)      Geza alikuwa anamiliki gari!! (Uk. 67)
b)      Nikahangaika huku na kule!!! (Uk. 15)
c)      Hakuwa Gezaa Yule hakika!! (Uk. 67)

iv.                Matumizi ya lugha ya kiingereza.
a)      Delete yes ……. No ……. (Uk. 81)
b)      One million (Uk. 4)
c)      Any way (Uk. 59)
d)     I’m sorry (Uk. 11)
e)      Big up (Uk. 73)
v.                  Matumizi ya lugha ya Kiarabu,
Wallah (Uk. 53)
UHAKIKI KWA KUTUMIA NADHARIA YA UHALISIA
Mambo ya msingi katika nadharia ya uhalisia yaliyojitokeza katika riwaya hii ni pamoja na:-  lugha rahisi isiyofikirisha, wahusika, matukio mahususi, ukweli, hakuna ufundi mkubwa wa kifani na demokrasia.
Lugha rahisi isiyofikirisha, lugha aliyotumia mwandishi ni lugha rahisi na yenye kueleweka kwa wasomaji kwani hajatumia lugha ya picha au ya mficho, viwango vyote vya elimu wanaweza kusoma na kuelewa.
Wahusika, msanii ametumia wahusika wanaosadifu uhalisia katiak jamii. Mfano, kama Khalfani na Latipha katika mapenzi yao, suala la usaliti lililojitokeza kwa latipha katika jamii yetu ya leo wapo watu kama hao. Pia Khalfani anawakilisha watu wenye mapenzi ya dhati katika jamii ya leo, hivyo mwandishi ametumia wahusika wenye kuonesha uhalisia.
Matukio mahususi, mwandishi ameyapangilia matukio katika uhalisia kutokana na kuwa matukio yaliyojitokeza katika riwaya hii ni kama vile utekaji wa gari, Khalfani kupelekwa mahabusu bila kuelewa kosa lake, kupewa kichapo na ndugu wa Latipha, kutekwa kwa mke wa Baisar na watoto ambapo mambo kama haya yanawakumba watu katika jamii yetu ya leo.
Ukweli, mwandishi wa riwaya hii ameonesha ukweli kuanzia mwanzo hadi mwishoni mwa riwaya hii ya fedheha, kwani mambo yaliyojitokeza kama vile:- rushwa, kubambikizwa kesi, usaliti, wivu kupita kiasi katika mapenzi na usafirishaji wa madawa ya kulevya ndivyo yalivyo katika jamii yetu ya leo.
Demokrasia, suala la haki kwa kiasi limejitokeza katika riwaya hii mfano, baada ya Baisar kuainisha wazi mambo yake aliyokuwa anawafanyia wananchi, alipelekwa mahakamani na kufungwa kifungo cha maisha. (Uk. 106)
Haukuna ufundi mkubwa wa kifani, wanauhalisia wanalenga zaidi kipengele cha maudhui kuliko fani kwani maudhui hulenga zaidi mambo yanayojiokeza katika jamii. Hivyo basi riwaya hii imelenga zaidi maudhui kuliko fani.
Kwa ujumla riwaya hii ya Fedheha imesadifu hali halisi ya maisha ya Tanzania, kutokana na mambo yaliyojadiliwa na matokeo ya mambo hayo. Hivyo mwandishi wa riwaya hii amefaulu kwa kiasi kikubwa kuakisi maisha ya nchi zinazo endelea hususani Tanzania.

Comments

Popular posts from this blog

notes za malenga wapya,uhakiki wa shairi la malenga wapya.

Semantiki kama taaluma nyingine ina mahusiano na taauma nyingine kama ifuatavyo katika mchoro na hatimaye katika maelezo yanayo eleza vipengele mbalimbali vya lugha:-

maana ya sintaksia,uhusiano wa sintaksia na matawi mengine,malengo ya sintaksia au isimu miundo, vipashio vya lugha ni vipi?,